


Ni globu ya kijamii inayojihusisha na mambo yote ya kijamii,natumaini jamii yangu ya kitanzania itafaidika sana pindi ichukuapo fursa ya kuperuzi kwenye globu hii,dhamira yangu ni kufikisha ujumbe pamoja na kuiburudisha jamii yangu na furaha yangu ni kuona natimiza dhamira yangu kwako.natumaini kuwa wewe utaniunga mkono kwa kile ambacho nataka kukifanya kwa ajili ya jamii yangu ya kitanzania.NASHUKURU KWA KUNIELEWA.
Ismail Ngayonga na Magreth Kinabo
MAELEZO
Dar-Es-Salaam
SERIKALI imekitaka Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) kuzingatia masharti ya usajili waliopewa na malengo waliyojipangia pasipo kuingilia masuala ya kisiasa nchini, ikiwemo kuzingatia suala la utawala bora.
Hayo yamesemwa leo Jijini Dar-Es-Salaam na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, Seth Kahumanda wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na tamko (TAMWA) juu ya taarifa ya vyombo vya ulinzi na usalama lilivyotolewa hivi karibuni na Mnadhimu Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ya Wananchi wa Tanzania( JWTZ ) Luteni Jenerali Abdulrahman Shimbo, utafiti wa taasisi ya Synovate pamoja na REDET.
Kamuhanda alisema kuwa Serikali inashangazwa na Kauli ya Mkurugenzi wa TAMWA, Analilea Nkya kwa kuwa imekwenda kinyume na majukumu ya taasisi hiyo, ambayo ni pamoja na kusaidia waandishi wanawake kujiendeleza kitaaluma ili kushika hatamu ya uongozi katika vyombo vya habari, kubadilisha mfumo wa habari hasi za wanawake na kuwasaidia wanawake Watanzania kujiletea maendeleo.
Aliongeza kuwa TAMWA ni chama cha kitaaluma kama vilivyo vyama vingine, na iwapo kinahitaji kubadili malengo yake kuwa ya 0kisiasa basi hakina budi kuangalia mustakabali wa chama chao na mwelekeo wao na kufuata utaratibu kwa mujibu wa sheria .
“Matamko ya Mkurugenzi wa TAMWA yamevuka mipaka na kwenda nje ya malengo ya TAMWA. TAMWA inatakiwa kuheshimu masharti ya usajili wao na kuyatekeleza,” alisema Katibu Mkuu huyo huku akisisitiza kwamba chama hicho pia kinatakiwa kuheshimu masuala ya utawala bora uliopo nchini kwa kuwa suala la kuheshimu misingi ya utawala bora si la Serikali pekee.
Kwa mujibu wa Kamuhanda alisema kuwa chama hicho bado kinakabiliwa na changamoto mbalimbali za utekelezaji wa malengo yake ikiwemo kuwaendeleza waandishi wa habari wanawake kwa ajili ya kuwapatia ujuzi wa kutosha utakaowawezesha kushika nafasi za uongozi katika vyombo vya habari na sehemu nyinginezo za maeneo ya kazi.
Aidha Kamuhanda aliongeza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na chama hicho, katika malengo yao waliojiwekea.
Akizungumzia kuhusu mwenendo wa vyombo vya habari juu ya mchakato wa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31,mwaka huu, Kahumanda alivishukuru baadhi ya vyombo vya habari na wahariri wake kwa kukemea matendo na kauli zinazoashiria kuhatarisha uvunjifu wa amani nchini.
“ Vyombo vya habari vinafanyakazi nzuri katika kuhabarisha wananchi juu ya mchakato wa Uchaguzi Mkuu baadhi yake vimepinga na kukemea waziwazi juu ya vitendo vinavyoashria uvunjifu wa amani kwa mfano kwa kuandika tahariri ninavipongeza kwa kuwa vimeonyesha ujasiri na ninaomba viendelee na msimamo huo kwa sababu amani ndio hazina kubwa ya nchi yetu,” alisisitiza Kamuhanda.
Awali akimkaribisha Katibu Mkuu ambaye alikuwa kwenye ziara ya kuitembelea Idara ya Habari(MAELEZO), Mkurugenzi wa Idara hiyo, Clement Mshana alisema ofisi zaidi zinahitajika kwa ajili ya kuhifadhi picha, machapisho mbalimbali na habari, hotuba za viongozi pamoja na vipindi mbalimbali ambavyo ni vya radio na televisheni ili viweze kutumika katika sehemu za baadae endapo janga la moto likitokea.
Mkurugenzi huyo aliongeza kuwa idara hiyo inaratibu shughuli za tovuti ya wananchi ambapo mpaka sasa wananchi kadhaa wwaliokuwa na kero zao zimewezwa kutatuliwa na kupatiwa majibu kutoka mamlaka husika.
- Waiaga CUF na kuchukua kadi za CCM
- Waahidi wengi zaidi wanakuja nyuma yao visiwani humo
Wakongwe wawili wa siasa za vyama vingi visiwani Zanzibar Mheshimiwa Fatma Maghimbi na Juma Othman Juma wamerudisha kadi zao za CUF na kuchukua za CCM leo jimboni Kawe jijini Dar es salaam na kuahidi wenzao wengi watafuata nyayo zao kutoka CUF.
Akielezea sababu zake za kurudi CCM, Juma Othman Juma amesema ameguswa kwa kazi kubwa aliyofanya Mheshimiwa Kikwete Tanzania Bara na Visiwani hususan aliporejesha amani na utulivu visiwani Unguja na Pemba kipindi cha uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
Alisema tangu historia ya vyama vingi ianze Tanzania, kila wakati wa uchaguzi wananchi wengi wa visiwa vya Unguja na Pemba hulazimika kukimbia visiwani humo kwa kuhofia hali ya kutokuwa na usalama katika kipindi hicho.
"Lakini sasa napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Kikwete kwa kurudisha heshima ya nchi yetu duniani kwani mwaka huu wa kampeni, hakuna hata mmoja aliyehama visiwani humo kukimbia uchaguzi" alimaliza Juma Othman akishangiliwa na umati mkubwa wa wana CCM waliojitokeza kwenye mkutano huo wa kampeni.
Mama Fatma Maghimbi amewahi kuwa waziri kivuli wa Katiba na Sheria ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwa kama mbunge wa Chama Cha Wananchi CUF. Naye Juma Othman Juma amewahi kuwa muanzilishi wa Chama Cha Siasa visiwani kabla ya kujiunga na Chama cha Wananchi CUF.
Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama cha Mapinduzi CCM Mh. Jakaya Kikwete akimnadi Mama Kizigha, mgombea ubunge wa CCM jimbo la kawe leo kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika kwenye viwanja vya Tanganyika Parkers jijini Dar es salaam. Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge, na Madiwani unatarajiwa kufanyika Oktoba 31 mwaka huu nchini kote. (Picha na Muhidin Issa Michuzi) |
sehemu ya nyomi uwanja wa Tanganyika Packers, Kawe, jijini Dar leo |