
Timu ya Simba leo imeibanjua timu ya Africa Lyon magoli mawili kwa bila kwenye uwanja wa Uhuru katika uzinduzi wa ligi kuu ya Vodacom iliyoanza leo jijini Dar es salaam, timu hiyo ilifanya umafia huo huku mashabiki mwake wakiishangilia kwa nguvu kwenmye uwanja huo. Alikuwa ni mchezaji mpya wa timu hiyo aliyetokea kwa watani wao wa jadi timu ya Young African ya mtaa wa Jangwani jijini Dar es salaam Amir Maftaha wakati alipoandika goli la kwanza katika dakika ya kumi na nne ya mchezo huo katika kipindi cha kwanza cha mchezo huo. Mpaka mapumziko Simba ndiyo ilikuwa ikiongoza goli 1-0 katika mchezo huo uliofungua pazia la ligi kuu ya Vodacom huku mahasimu wao wakuu timu ya Yanga ikiifunga timu ya Polisi Dodoma goli 1-0 kwenye uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma. Katika kipindi cha pili Amir Maftaha tena alifunga goli la pili katika dakika ya sitini na nne ya mchezo na kuifanya timu ya Simba kuibuka na magoli 2-0 hivyo kuifanya timu ya Africa Lyon kuondoka uwanjani ikiambulia patupu, ushindi huo wa timu ya Simba unaipa pointi tatu za mwanzo katika ligi hiyo.
No comments:
Post a Comment